Katibu Tawala Mkoa wa Tanga atembelea Ujenzi wa Madarasa
Katibu Tawala Mkoa Tanga Bi. Pili Mnyema ametembelea Mradi wa Ujenzi wa Vyumba vya Madarasa katika Shule za Msingi zilizopo Halmashauri ya Mji wa Korogwe. Ujenzi huo wa Vyumba vya Madarasa unatekelezwa chini ya Mradi wa BOOST kwa thamani ya Shilingi Milioni Mia Sita Sabini na Nne na Laki Moja (674,100,000.00/=). Ziara hiyo ilifanyika Julai 04, Mwaka huu katika maeneo mabalimbali ya Mji wa Korogwe.
“Natoa pongezi kwa Mkurugenzi na Wataalamu wote kwa usimamizi mzuri wa Ujenzi wa Madarasa” alisema Bi. Pili Mnyema ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga wakati akikagua Ujenzi wa Vyumba vya Madarasa katika Mji wa Korogwe. Bi. Pili alifafanua kuwa Serikali chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan imejipanga vyema katika uboreshaji wa Miundombinu ya Elimu ili Wanafunzi waweze kusoma katika mazingira mazuri.
“Tunashukuru Katibu Tawala kutembelea Mji wa Korogwe ili kuona hatua mbalimbali tulizofikia katika utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Vyumba vya Madarasa” alisema Bw. Tito Mganwa ambaye ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe. Bw. Tito alisisitiza kuwa Halmashauri itahakikisha inatekeleza Mradi wa Ujenzi wa Vyumba vya Madarasa kwa kufuata kanuni na taratibu zote za ujenzi ili kufikia lengo la Serikali katika uboreshaji wa elimu.
Korogwe Tanga Tanzania
S.L.P: 615 Korogwe
Simu: 0272650050
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@korogwetc.go.tz
Copyright©2018 Korogwe Town Council. All rights reserved.